corona

Mamlaka ya kisiwani Zanzibar imetangaza siku ya Jumapili, Aprili 05 kuwa na maambukizi mapya ya watu wawili na hivyo kufanya kisiwa hicho kuwa na watu saba wenye maradhi ya corona.

Wagonjwa wote wanaendelea na matibabu huku hali zao za afya zikiwa zinaendelea vizuri.

Mgonjwa wa kwanza ana umri wa miaka 33, aliingia Zanzibar tarehe 18, Machi 2020 akiwa anatokea Tanga na mgonjwa wa pili ana miaka 27, alirejea kutoka mapumziko Tanga Machi 13, 2020 .

Maofisa wa afya wanaendelea kufuatilia watu wote waliohusiana na wagonjwa hao.

Idadi hiyo mpya inafanya Tanzania kuwa na idadi ya wagonjwa 22 wa corona.

Serikali ya Tanzania imeamua kuanzia sasa kuwa wageni wote watakaowasili Tanzania watakaa karantini katika hosteli za chuo kikuu cha Dar es Salaam.

Image caption

Waziri wa Afya Tanzania Ummy Mwalimu amewataka wananchi kujihadhari

Wizara ya Afya nchini Tanzania Jumatano Aprili 1 imetangaza ongezeko la mgonjwa mmoja wa virusi vya corona nchini humo hali inayofikisha idadi ya wagonjwa nchini humo kufikia 20.

Kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Afya Ummy Mwalimu, mgonjwa huyo ni mwanamke mwenye miaka 42 na raia wa Marekani.

Taarifa ya Bi Mwalimu inaeleza kuwa mgonjwa huyo mpya alikuwa karibu na mtu aliyesafiri nje ya nchi na baadaye kuthibitika kuwa ana maambukizi ya virusi hivyo baada ya kurejea Tanzania.

Katika taarifa hiyo bi Ummy pia amethibitisha kuwa tayari wagonjwa wawili nchini humo wamepona virusi hivyo.

“…Tarehe 31 Machi, mmoja kati ya wagonjwa waliokuwa katika kituo cha matibabu cha Temeke Dar es Salaam amethibitika kupona maambukizi aliyokuwa nayo na ameruhusiwa kurudi nyumbani na hivyo sasa kufanya jumla ya watu waliopona kuwa wawili,” imeeleza taarifa ya waziri Ummy.

Jana Jumanne Tanzania ilitangaza kifo cha kwanza cha mgonjwa wa virusi vya corona nchini humo.

Mpaka sasa kwa mujibu wa waziri kuna wagonjwa 17 ambao bado wanaendelea na matibabu na hali zao zipo vizuri.

Jumatatu wiki hii waziri Ummy alibainisha kuwa serikali imekuwa ikufatilia “watu wote wa karibu waliokutana na wagonjwa (contact tracing),” na kuwataka wananchi wote kuendelea kuchukua tahadhai ili kujikinga na ugonjwa huu,” ameeleza Bi Mwalimu.

Siku hiyo alitangaza wagonjwa watato, watatu kutoka Dar es Salaam na wawili kutoka Zanzibar.

Image caption

Kama njia moja ya tahadhari, ndoo za maji ya kunawa zimetawanywa katika maeneo mbali mbali ya Tanzania.

Nchini Tanzania, wagonjwa wa virusi hivyo wamebainika kutoka Dar es Salaam, Zanzibar, Arusha na Kagera.

Kutokea Januari 1 mpaka sasa zaidi ya wasafiri milioni 1.8 wamefanyiwa ukaguzi kwa kupimwa joto la mwili katika vituo vya mipaka 27 ikiwemo viwanja vya ndege na bandari.

Wakati idadi ikipanda nchini Tanzania, nchi jirani za ukanda wa Afrika Mashariki pia hali inaendelea kuwa mbaya.



Source link